Simba hiyooo Robo Fainali Ligi ya Mabingwa Afrika

Ushindi wa mabao 4-1 tuliopata dhidi ya AS Vita kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa leo, umetufanya kuingia kwa kishindo hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Matokeo hayo yanatufanya kufikisha alama 13 tukisalia kileleni mwa kundi A tukijihakikisha kubaki kwani hakuna timu itakayofikisha pointi hizo.

Katika mchezo wa leo, Luis Miquissone alitupatia bao la kwanza dakika ya 30 baada ya kupokea pasi kutoka kwa Bernard Morrison akiwa ndani ya 18.

Bao hilo lilidumu kwa dakika mbili kufuatia Vita kusawazisha kupitia kwa Zemanga Soze baada ya kupokea pasi ya Merville Kikasa aliyepiga akiwa ndani ya 18.

Clatous Chama alitupatia bao la pili dakika ya 45 akipokea mpira kutoka kwa Mohammed Hussein aliyempiga chenga mlinzi mmoja wa Vita kabla ya kuachia shuti la chini chini lililotinga moja kwa moja wavuni.

Rally Bwalya alitupatia bao la tatu kwa shuti kali nje kidogo ya 18 dakika ya 66 baada ya kupokea pasi kutoka kwa Chama.

Chama alikamilisha karamu ya mabao baada ya kutupia la nne dakika ya 83 akimaalizia pasi ya Miquissone.

Kocha Didier Gomez aliwapumzisha Chris Mugalu, Morrison, Jonas Mkude, Chama na Miquissone na kuwaingiza Medie Kagere, Bwalya na Erasto Nyoni, Hassan Dilunga na Francis Kahata.

SHARE :
Facebook
Twitter

2 Responses

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

GET NEWSLETTER