Mlinzi wa kati, Joash Onyango amekabidhiwa Tuzo yake ya Mchezaji Bora wa Mwezi Machi wa Mashabiki (Emirate Simba Fans Player of the Month) na hundi ya Sh 1,000,000 kutoka kwa wadhamini Emirate Aluminium.
Onyango ameshinda tuzo hiyo baada ya kuwashinda Luis Miquissone na mlinda mlango Aishi Manula kutokana na kura nyingi zilizopigwa na mashabiki kupitia Tovuti hii ya Klabu.
Raia huyo wa Kenya amekabidhiwa tuzo hiyo katika viwanja vyetu ya Mo Simba Arena baada ya kumalizika kwa mazoezi ya asubuhi.
Ofisa Mahusiano na Masoko wa Emirate Aluminium, Issa Maeda aliyekabidhi tuzo hiyo amesema anaamini ushirikiano huu utaendelea kwa muda mrefu zaidi kutokana na mahusiano yaliyopo.
"Leo tumemkabidhi Onyango tuzo hii na hundi ikiwa ni zawadi ya kuchaguliwa mchezaji bora wa Mwezi Machi kwa mujibu wa mkataba wetu na Simba," amesema Maeda.
Kwa upande wake Onyango amewashukuru mashabiki kwa kumpigia kura nyingi na wadhamini Emirate Aluminium kumpa tuzo hiyo ambayo inamuongezea nguvu ya kupambana zaidi.
"Nawashukuru mashabiki wetu kwa kunipigia kura nyingi pamoja na wadhamini Emirate Aluminium kwa kunipa tuzo hii. Nawahakikishia nitaendelea kupambana kuhakikisha naisaidia timu kufanya vizuri zaidi," amesema Onyango.
Katika kinyang'anyiro hicho, jumla ya kura zilizopigwa ni 25,719 ambapo Onyango amepata kura 20,288 sawa na asilimia 79, Manula kura 4,673 sawa na asilimia 18 na Miquissone kura 758 sawa na asillimia 2.