Simba Sports Club
News

Kapombe, Zimbwe Jr waongezwa Stars

26 Mar 2023 By simbasc 277 views
Walinzi wetu wawili wa pembeni, Shomari Kapombe na Mohamed Hussein 'Zimbwe Jr' wameongezwa katika kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' inayojiandaa na mchezo wa marudiano wa kufuzu fainali za Afrika (AFCON) dhidi ya Uganda 'The Cranes' utakaopigwa Jumanne Uwanja wa Benjamin Mkapa. Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia ametangaza suala hilo mbele ya Waandishi wa Habari wakati zoezi la kukabidhi tiketi za mashabiki zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na zile zilizotoka Wiraza ya Utamaduni na Michezo. Wiki iliyopita kocha mkuu wa Taifa Stars, Adel Amrouche alikutana na walinzi hao na kuzungumza nao kwa kirefu baada ya mchezo wetu wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Horoya tulioibuka na ushindi wa mabao 7-0. Tayari Kapombe na Zimbwe Jr wamejiunga na kambi ya Taifa Stars na klabu imewapa baraka zote kwa ajili ya kwenda kutetea bendera ya nchi. Kapombe na Zimbwe Jr wanaungana na walinda milango Aishi Manula na Beno Kakolanya pamoja na kiungo Mzamiru Yassin ambao wametoka kikosini kwetu.
Advertisement
Back to homepage
Share this story