Baada ya kufanikiwa kutinga Fainali ya Michuano ya Azam Sports Federation Cup kwa kuifunga Azam FC bao moja, Kocha Mkuu Didier Gomes amesema anakiamini kikosi chetu kuwa ni bora na wachezaji huwa wanajituma.
Gomes amesema msimu huu tuna timu imara kulinganisha na nyingine na kila tunapoingia uwanjani tunapewa nafasi kubwa ya kushinda ingawa kwenye mpira kuna matokeo matatu.
Akizungumzia mchezo dhidi ya Azam, Gomes amesema kipindi cha kwanza tulicheza aina ya soka tuliozea lakini cha pili ilibidi tutumie mipira mirefu sababu ya wapinzani na uwanja haukuwa rafiki na ndiyo sababu ya kuwaingiza Medie Kagere na Bernard Morrison.
Raia huyo wa Ufaransa ameongeza kuwa mchezo wa leo umeamuliwa zaidi na uwezo wa kujituma kwa wachezaji kuliko mbinu kwa kuwa nguvu ilitumika zaidi.
"Nakiamini sana kikosi changu, Simba ni moja ya timu ambayo ina kikosi bora zaidi msimu huu, tulijua tutapata ushindani mkubwa kutoka kwa Azam lakini tulikuwa tumejipanga kushinda.
"Kama nilivyosema huko nyuma malengo yetu msimu huu ni kuchukua mataji yote ya ndani na tunakaribia kuchukua ligi na leo tumeingia fainali FA ngoja tuone itakuwaje huko mbele," amesema Gomes.