Kikosi chetu leo kitashuka katika Uwanja wa Benjamin Mkapa saa moja kuikabili Mtibwa Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC.
Tunaingia katika mchezo wa leo tukiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mechi iliyopita lakini haijarudisha nyuma morali ya wachezaji wetu.
Tunajua mchezo utakuwa mgumu na tunaiheshimu Mtibwa ambayo ipo kwenye kiwango bora kwa sasa lakini tumejipanga kuhakikisha tunabakisha pointi tatu nyumbani.
KOCHA MGUNDA
Kocha Mkuu Juma Mgunda amesema maandalizi ya mchezo yamekamilika na wachezaji wapo kwenye hali nzuri kupambania alama tatu.
Mgunda amesema kila mchezo una mbinu zake na maandalizi yake, mapungufu ya mechi iliyopita yameonekana na yamefanyiwa kazi mazoezini na mazuri yataendelezwa.
“Kikosi kiko tayari kwa mchezo wa kesho, tunaiheshimu Mtibwa ni timu nzuri ina wachezaji wazuri na ipo kwenye kiwango bora kwa sasa lakini tumejiandaa kupambana kupata ushindi,” amesema Mgunda.
ZIMBWE JR AFUNGUKA
Nahodha Msaidizi Mohamed Hussein ‘Zimbwe Jr’ amewaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanjani kuipa sapoti timu ambapo ameahidi kuwapa furaha.
“Sisi kama wachezaji tupo tayari kwa mchezo, tunajua mchezo utakuwa mgumu tunategemea kupata upinzani lakini tumejipanga kushinda, kikubwa tunawaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi kutupa sapoti,” amesema Zimbwe Jr.
JIMMYSON, OKWA KUIKOSA MECHI
Katika mchezo wa leo tutakosa huduma ya wachezaji wawili; Jimmyson Mwanuke na Nelson Okwa ambao bado ni majeruhi.