Phiri atupia mawili tukiifunga Coastal Mkwakwani

Mshambuaji kinara Moses Phiri amefunga mabao mawili katika ushindi wa 3-0 tuliyowafunga Coastal Union katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliopigwa Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga.

Mabao hayo yanamfanya Phiri kufikisha 10 na kuwa sawa na anayeongoza katika orodha ya wafungaji kwenye Ligi Kuu mpaka sasa.

Mchezo huo ulianza kwa kasi ya kawaida huku timu zikitumia dakika 15 za mwanzo kusomana huku mpira ukichezwa zaidi Katikati ya uwanja.

Walinda milango wa timu zote hawakupata kashikashi nyingi katika kipindi cha kwanza kutokana na mashambulizi mengi kuishia kwa walinzi.

Phiri atupia bao la kwanza dakika ya 53 kwa shuti kali ndani ya 18 baada ya kumpiga chenga mlinzi mmoja wa Coastal akimalizia pasi ya Clatous Chama.

Dakika ya 61 Phiri alitupatia bao la pili kwa mkwaju wa penati kufuatia Shomari Kapombe kufanyiwa madhambi na mlinzi wa kati wa Coastal, Lameck Lawi ndani ya 18.

Chama alikamilisha karamu ya mabao kwa kufunga la tatu dakika ya 89 kufuatia shuti la Phiri kuokolewa na mlinda mlango kabla ya mpira wa kichwa wa John Bocco kugonga mwamba wa juu na kumkuta nyota huyo akiwa anatazamana na nyavu.

Kiungo mkabaji, Sadio Kanoute alitolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 90 kufuatia kadi ya pili njano baada ya kumchezea madhambi mchezaji wa Coastal.

Kocha Juma Mgunda aliwatoa Aishi Manula, Pape Sakho, Bocco na Henock Inonga na kuwaingiza Benno Kakolanya, Augustine Okrah, Vincent Akpan na Mohamed Ouattara.

SHARE :
Facebook
Twitter

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

GET NEWSLETTER