Kwaheri ‘kitasa’ Pascal Wawa

Uongozi wa klabu umempa mkono wa kwa heri mlinzi wa kati Pascal Serge Wawa, raia wa Ivory Coast ambaye anamaliza mkataba wake mwishoni mwa msimu huu.

Wawa atacheza mchezo wake wa mwisho akiwa na kikosi chetu Juni 23, dhidi ya Mtibwa Sugar utakaofanyika Uwanja wa Benjamin Mkapa ambapo tutautumia kumuaga rasmi.

Baada ya mchezo huo, Wawa hatakuwa sehemu ya kikosi kitakachosafiri kwenda Nyanda za juu Kusini kwa ajili ya mechi zetu mbili zilizobaki za kumalizia msimu dhidi ya Tanzania Prisons na Mbeya Kwanza.

Wawa amedumu nasi kwa kipindi cha misimu minne akituwezesha kuchukua ubingwa wa Tanzania bara mara nne mfululizo, ubingwa wa Kombe la Shirikisho la Azam Sports mara mbili, Ngao ya Hisani mara tatu na Kombe la Mapinduzi.

Tukiwa na Wawa tumefanikiwa kucheza robo fainali tatu za michuano ya Afrika ikiwemo robo fainali mbili za Ligi ya Mabingwa na moja ya Kombe la Shirikisho.

Uongozi unapenda kumshukuru Wawa kwa utumishi wake uliotukuka ndani ya klabu yetu na kwa kuthamini mchango wake Alhamisi tutamuaga mbele ya mashabiki kama ilivyo kawaida yetu.

‘Merci beaucoup Pascal Wawa’

SHARE :
Facebook
Twitter

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

GET NEWSLETTER